PLAN INTERNATIONAL YACHANGIA VIFAA VYA ELIMU RUKWA

 


 

Shirika la Plan International Tanzania limekabidhi msaada wa vitabu, vyoo shirikishi na miundombinu ya maji kwa shule za sekondari na msingi kwenye Halmashauri za Wilaya  Nkasi, Kalambo na Sumbawanga vyenye thamani ya shilingi Milioni 786 .

 


Halfa ya makabidhiano ya msaada huo imefanyika katika shule ya msingi Milundikwa wilaya ya Nkasi jana (Januari 19,2023) ambapo Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga Sebastian Waryuba alipokea msaada huo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Queen Sendiga.

 

Waryuba akizungumza kwenye hafla hiyo alitoa pongezi kwa shirika hilo kwa kuchangia vyoo shirikishi 17 na miundombinu ya maji katika shule za msingi 7 na sekondari 9 katika Wilaya za Nkasi, Sumbawanga Vijijini na Kalambo vyenye jumla ya thamani ya shilingi  za kitanzania 716, 607, 527.

 


 Plan International imetoa pia  vitabu vya kiada 10, 128 kwa shule za msingi 29  za wilaya ya Nkasi vyenye thamani ya shilingi za kitanzania 70, 210, 000 vitakavyotumika kufundishia na kujifunzia wanafunzi na walimu.

 

“Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa unaofanywa na Shirika la Plan International kwa kushirikina na Serikali katika kujenga uwezo na kuboresha upatikanaji wa elimu bora kwa shule za msingi na awali katika Mkoa wa Rukwa na kuleta maendeleo ya watanzania katika sekta mbalimbali za kijamii, alisema Waryuba.

 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Plan International Tanzania  Mona Girgis alisema lengo la shirika ni kuhakikisha elimu bora inatolewa kwa wanafunzi hususan watoto wa kike ndio maana linashirikiana na serikali kuboresha miundombinu ikiwemo vyoo bora na safi na vitabu.

 


Mkurugenzi huyo alisema pia shirika limefanikiwa kutoa mafunzo ya kusoma, kuandika na kuhesabu (KKK)  kwa walimu wa darasa la kwanza na la pili wapatao 48 kutoka shule za msingi 22 zilizopo kwenye kata 5 za Nkandasi, Mashete, Mkwamba, Kate na Mtenga wilaya ya Nkasi.

 


Kwa upande wake Angela Kayawe ( 14) mwanafunzi wa Darasa la Saba shule ya msingi Milundikwa alitoa shukrani kwa shirika la Plan International kwa msaada walioutoa utakaosaidia kuimarisha taaluma mingoni mwa wanafunzi.

 



Comments

Popular posts from this blog

Watumishi Wa Umma Wilayani Kalambo Waungana Kuadhimisha Kumbukizi Ya Mashujaa Kwa Kufanya Usafi.

Dc Kalambo Ataka Walio Husika Kumuozesha Mwanafunzi Wa Darasa La Saba Kukamatwa

Mkurugenzi UTPC awataka Waandishi kuandika Habari za Usawa wa kijinsia ili kuleta mabadiliko Chanya katika jamii.